Adverts

Nov 30, 2010

PINGAMIZI LA UBUNGE IRINGA MJINI LATINGA MAHAKAMANI


Katibu wa mheshimiwa Monica Mbega bwana Charles Charles akizungumzia pingamizi lililowekwa dhidi ya Mchungaji Msigwa(picha kwa hisani ya francis godwin blog)

MBUNGE wa zamani wa jimbo la Iringa mjini na mkuu wa mkoa wa KIlimanjaro ambaye alikuwa mgombea ubunge jimbo la Iringa mjini kupitia chama cha Mapinduzi (CCM) Monica Mbega amefungua kesi namba 3 ya mwaka 2010 katika mahakama kuu kanda ya Iringa akipinga matokeo yaliyompa ushindi mgombea mbunge wa chama cha Demokrasia na maendeleo (chadema) mchungaji Peter Msigwa.




Katibu wa CCM wilaya ya Iringa mjini Charles Charles alithibitisha mbele ya waandishi wa habari leo ofisini kwake kuhusiana na Mbega kwenda mahakamani kupinga ushindi wa mchungaji Msigwa wa Chadema kwamadai ya kuwepo kwa kasoro zaidi ya 10 zilizopata kujitokeza siku ya uchagua mkuu octoba 31 ikiwemo ya vituo vya kupigia kura kuhamishwa dakika za mwisho na kufanya baadhi ya wapiga kura kutopiga kura.



Kasoro nyingine ni ile ya tofauti ya matoke yaliyotangazwa na msimamizi wa uchaguzi jimbo la Iringa mjini ambayo kwa mujibu wa Mbega kuwa yalionyesha kutofautiana kwa kura kama 800 na sehemu ila matokeo ya pili yaliyotangzwa bila kuwepo kwa wakala wala mgombea wa CCM yanaonyesha mgombea huyo wa CCM alipitwa kwa kura zaidi ya 2000 na mgombea wa Chadema.



Hivyo alisema kuwa kutokana na kasoro hizo na nyingine nyingi mgombea huyo wa CCM Mbega amelazimika kwenda mahakamani kupinga matokeo hayo ya uchaguzi mkuu .



Charles alisema kuwa matokeo ya kwanza ya ubunge yaliyotangazwa na msimamizi wa uchaguzi yalionyesha mgombea wa NCCR-mageuzi Mariam Mwakingwe alikuwa amepata kura 950 na Monica Mbega (CCM) alikuwa amepata kura 16,916 huku mchungaji Msigwa akipata kura 17742 na kuwa matokeo hayo yalitangazwa huku mawakala wa CCM wakiwepo na kupokea hivyo.



Japo baadaye msimamizi wa uchaguzi alitangaza matokeo mapya ambayo mgombea wa CCM wala wakala wake hakuwepo ambapo matokeo hayo Msigwa yalimpa ushindi mkubwa Msigwa kwa kupata kura 17,352 wakati Mgombea waNCCR Mageuzi Mwakingwe akipata kura 1292 .



Hivyo alisema kuwa ukitazama matokeo hayo unapata picha halisi ni jinsi gani ambavyo msimamizi wa uchaguzi alivyoshindwa kutoa matokeo sahihi ya jimbo hilo na kuwa hadi sasa mgombea wa CCM hajapata nakala ya matokeo hayo mapya ambayo ndiyo yamempeleka Msigwa bungeni.



Pia alisema kuwa kasoro nyingine ni ile ya idadi ya wapiga kura katika baadhi ya vituo kuonekana kubwa zaidi ya wale waliojiandikisha na sehemu nyingi idadi ya waliopiga kura na wasio piga kura ukijumlisha unakuta kuna tofauti kubwa ya kura kuzidi.



Hata hivyo alishindwa kutaja wakili anayesimamia kesi hiyo kwa madai kuwa atajulikana pindi kesi hiyo itakapoanzwa kusikilizwa pamoja na kujua idadi ya halisi ya kasoro zilizotolewa na Mbega ambaye hakuweza kupatikana kuelezea suala hilo.



Kwa upande wake Mchungaji Msigwa alipoulizwa kuhusiana na madai hayo ya Mbega kwenda Mahakamani kupinga ushindi wake alisema kuwa hata yeye amekuwa akisikia kuwepo kwa suala hilo japo hadi jana alikuwa hajapatakufikishiwa taarifa yoyote rasmi toka mahakamani juu ya kuwepo kwa kesi hiyo.



"Mimi mwenyewe nimekuwa nikisikia kama Mbega amekwenda mahakamani kupinga ushindi wangu ila mimi sijapata taarifa rasmi za kuitwa mahakamani japo ni haki yake ya msingi kwenda mahakamani"alisema Mbunge Msigwa alipoulizwa kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi.



indaba2010