Adverts

Oct 25, 2011

UFARANSA KUISAIDIA KENYA KUPAMBANA NA AL SHABAAB

Ufaransa itatoa msaada wa vifaa kwa majeshi ya Kenya yanayopambana na wanamgambo wa kiislamu katika mpaka na Somalia, msemaji wa jeshi la Ufaransa alisema. Kanali Thierry Burkhard alisema ndege za Ufaransa zitasafirisha vifaa vya kijeshi kwa askari wa Kenya karibu na mpaka wa Somalia. Taarifa zinazohusianaKenya, Somalia, Ghasia, alshababRais wa Somalia Sheikh Sharif Ahmed amelaani hatua ya Kenya kuingia Somalia kwa minajil ya kupambana na kundi la al-Shabab. Kanali Burkhard amekana madai ya jeshi la Kenya kwamba meli ya kivita ya Ufaransa ilishambulia mji mmoja wa Somalia siku ya Jumamosi. Dhamira ya KenyaKanali Burkhard alisema harakati za Ufaransa "zina upeo mdogo", shirika la habari la AP limeripoti. Alisema kutashuhudiwa kwa ndege za Ufaransa zikisaidia jeshi la Kenya kusafirisha vifaa vya kijeshi kutoka mji mkuu, Nairobi, kwenye uwanja wa ndege karibu na mpaka wa Somalia. Siku ya Jumapili, msemaji wa jeshi la Kenya Meja Emmanuel Chirchir aliliambia shirika hilo la habari kwamba jeshi la majini la Ufaransa lilishambulia kwa mabomu mji wa Kuda katika pwani ya Somalia. Kanali Burkhard alikana madai hayo, akisema Ufaransa haina meli za kijeshi eneo hilo. Wiki iliyopita, al-Shabab lilipoteza udhibiti wa mji wa Ras Kamboni baada ya mashambulio yaliyofanywa na jeshi la majini la Kenya na wapiganaji wa eneo hilo. Kenya ilipeleka majeshi yake Somalia Oktoba 16 kulishambulia kundi la al-Shabab, ikisema imetishia utulivu wa nchi hiyo. Nairobi imelishutumu kundi hilo kwa kuhusika na utekaji nyara Kenya, ikiwemo ya mwanamke wa Kifaransa, Marie Dediieu, Oktoba 1. Bi Dedieu, aliyekuwa na saratani, alifariki dunia Somalia wiki iliyopita. Al-Shabab lilikana kuhusika na utekaji nyara huo.