Adverts

Dec 31, 2011

Rais Kikwete ateua makatibu wa Wizara!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Ijumaa, Desemba 30, 2011, amefanya uteuzi wa Makatibu Wakuu na Naibu Katibu Mkuu na pia amefanya uhamisho wa Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu kuanzia jana, Alhamisi, Desemba 29, 2011.



Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Bwana Phillemon Luhanjo, inasema kuwa Bwana Fanuel E. Mbonde, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Ikulu, anahamishiwa Wizara ya Katiba na Sheria, na Bwana Alphayo Kidata, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Ikulu, anahamishiwa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).



Aidha, taarifa hiyo inasema kuwa Bwana Eliakim C. Maswi, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini. Kabla ya uteuzi wake, Bwana Maswi alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kwa sasa anakaimu nafasi ya Katibu Mkuu, Nishati na Madini.



Mheshimiwa Rais Kikwete pia amemteua Bwana Peter Ilomo, Mratibu Mkuu wa Sera na Mipango, Ofisi ya Rais, Ikulu, kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Ikulu.



Naye Bibi Susan Paul Mlawi ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Ikulu. Kabla ya uteuzi huu, Bibi Mlawi alikuwa Msaidizi wa Katibu wa Baraza la Mawaziri (Cabinet Under Secretary) Kamati ya Katiba na Bunge ya Baraza la Mawaziri.



Taarifa ya Bwana Luhanjo inamalizia kwa kusema kuwa mabwana Maswi na Ilomo pamoja na Bibi Mlawi wataapishwa Jumatatu, Januari 2, 2012, saa nne asubuhi, Ikulu, Dar es Salaam. Imetolewa na: Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, DAR ES SALAAM. 30 Desemba, 2011