Adverts

Nov 15, 2013

OFISI YA TAKWIMU YATOA TAARIFA YA UMASKINI WA CHAKULA, VIJIJINI HALI NI MBAYA ZAIDI KULIKO MIJINI



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU  MATOKEO YA  UTAFITI WA MAPATO NA MATUMIZI YA KAYA BINAFSI (HBS) TANZANIA BARA 2011/12, TAREHE 14 NOVEMBA, 2013

Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Wizara ya Fedha iliendesha Utafiti wa Mapato na Matumizi ya  Kaya Binafsi Tanzania Bara katika mwaka 2011/12. Utafiti huu  ulikusanya, kuandaa na kuchambua taarifa za mapato, matumizi na manunuzi ya kaya

Matumizi ya Kaya Binafsi wa mwaka 2011/12 umelenga kutoa  viashiria vitakavyosaidia kufuatilia na kutathmini maendeleo ya  sekta mbalimbali zilizoainishwa kwenye  Mkakati wa Kukuza  Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA II) Tanzania.
Takwimu zilizokusanywa zilihusu watu na kaya katika maeneo  yafuatayo:
 Elimu na afya ya Wanakaya;
 Manunuzi na matumizi ya kaya;
 Umiliki wa vifaa na rasilimali;
 Makazi na vifaa vya ujenzi;
 Upatikanaji wa huduma na vifaa;
 Upatikanaji wa maji na usafi wa mazingira;
 Shughuli za kiuchumi na ajira;
 Utalii;
 Umiliki wa biashara zisizo za kilimo; na
 Shughuli za kilimo.
Utafiti huu ulifanyika kuanzia mwezi
Oktoba 2011 hadi Oktoba 2012 ambapo jumla ya kaya  10,186  kati ya 10,400 zilizokuwa zimelengwa zilihojiwa  kutoka katika maeneo ya Dar es Salaam, maeneo mengine  ya mjini na vijijini, Tanzania Bara.

Kila kaya iliyochaguliwa  ilihojiwa juu ya masuala yote yaliyotajwa hapo juu pamoja na  kujaza  kijitabu  cha kumbukumbu  ambacho kaya  ilitakiwa kuandika  mapato na matumizi ya kila siku kwa  muda wa siku 28 mfululizo. Kijitabu hiki cha kumbukumbu  kililenga katika kupata matumizi ya moja kwa moja (hasa chakula)  ya kaya pamoja na matumizi mengine yasiyo ya  chakula kwa kipindi hicho cha siku 28.

Matokeo  ya utafiti huu yanaonesha  kuwa  kiwango cha umaskini wa chakula na ule wa mahitaji ya msingi  ni tatizo zaidi kwa  Wananchi wa vijijini ikilinganishwa na Wananchi wanaoishi mjini hususan Dar es Salaam na maeneo mengine ya mjini. Wakati wastani wa kitaifa wa kiwango cha umaskini  wa chakula ni asilimia  9.7,  kiwango hicho kinafikia  asilimia 11.3 kwa maeneo ya vijijini.

Dar es Salaam ina  kiwango cha chini kabisa cha umaskini wa chakula cha asilimia  1.0 ambapo  Wananchi  anaoishi maeneo mengine ya mjini wana umaskini wa chakula wa asilimia 8.7.
Kwa upande wa umaskini wa mahitaji ya msingi, wastani wa  Tanzania Bara ni asilimia 28.2  kilinganishwa na asilimia 33.3  kwa maeneo ya vijijini na asilimia 21.7 kwa maeneo mengine  ya mjini. Dar es Salaam ina kiwango cha chini cha umaskini wa  mahitaji ya msingi cha asilimia 4.1.

Matokeo ya utafiti huu yanaonesha  jitihada za Serikali katika kuongeza ujenzi wa shule zaidi hasa
zile za sekondari ambazo zimewezesha kupanda kwa kiwango  cha wanafunzi wanaojiunga katika elimu ya sekondari  kwa  karibu mara mbili, kutoka asilimia 15 mwaka 2007 hadi  asilimia 29 mwaka 2011/12.


Matumizi ya nishati ya umeme katika maisha ya kila siku ya  Wananchi katika kaya ni eneo lingine ambalo Serikali imelenga kuliboresha katika jitahada zake za kuboresha maisha ya  Wananchi. Matokeo ya utafiti huu yanaonesha  kuwa  kaya zinazotumia umeme angalau kwa ajili ya mwangaza wa ndani  zimeongezeka kutoka asilimia 13  kwa mwaka 2007 hadi asilimia 18 kwa mwaka 2011/12