Adverts

Feb 7, 2011

RAIS JK AVUNJA UKIMYA KUHUSU DOWANS

RAIS JK AVUNJA UKIMYA KUHUSU DOWANS: " Ndugu Wana-CCM na Ndugu Wananchi; Jambo ninalotaka kulizungumzia sasa sikutaka kulizungumza kwa sababu Waziri Mkuu alishalifafanua baada ya semina ya Wabunge wa CCM na hata Mheshimiwa John Chiligati, Katibu wa Siasa na Uenezi Taifa alishalizungumzia. Sikuona umuhimu wa kufanya hivyo kwa sababu viongozi wenzangu hao wameelezea kwa ufasaha uamuzi wa Kamati Kuu na ule wa kikao cha pamoja cha Wabunge wa CCM.
Lakini, yapo maneno mengi ati mbona Rais yupo kimya sana, hatujamsikia kusema chochote? Niseme nini zaidi na hao wote wameshasema kwa niaba yangu. Wapo wanaosema nipo kimya kwa sababu nahusika na Downs na ati ndiyo mwenyewe hasa. Wapo wanaosema niko kimya au nashindwa kuchukua hatua, kwa sababu marafiki zangu wamehusika. Nawalinda. Kwa sababu hiyo, nikaona nami nisema angalau watu wanisikie lakini sina la ziada ni yale yale yaliyokwishasemwa.
Kwanza niseme wazi kwamba ule msemo wa wahenga wa akutukanae hakuchagulii tusi hapa umetimia. Napenda kuwahakikishia wana-CCM na wananchi wenzangu kuwa sina uhusiano wowote wa kimaslahi kwa namna yoyote ile na kampuni ya Dowans. Sina hisa zozote wala manufaa yoyote yale. Pia sina ajizi wala kigugumizi cha kuchukua hatua kwa sababu ya rafiki yangu au hata kama angekuwa ndugu yangu kahusika. Maamuzi yaliyofanywa na Kamati Kuu na Kamati ya Chama ya Wabunge wa CCM yalifanywa chini ya uogozi wangu. Ni uthibitisho tosha wa ukweli huo. Waliokuwepo kwenye vikao hivyo wanajua ukweli wa haya ninayosema. Ningekuwa na maslahi au hofu tusingefanya uamuzi ule.
Wana-CCM Wenzangu na Wananchi Wenzangu; Kama mtakavyokumbuka tulipoingia madarakani nchi ilikuwa na tatizo kubwa la ukame mkali sana ambao haujawahi kutokea. Mavuno ya chakula yalikuwa mabaya tukawa na njaa kali na watu 3,776,000 walilazimika kuhudumiwa na Serikali. Aidha, mito mikubwa na midogo ikapungukiwa sana maji na mingine kukauka kabisa. Matokeo yake ni mabwawa yetu yote ya kuzalisha umeme yakakosa maji hivyo uzalishaji wa umeme ukaathirika vibaya sana na nchi ilikuwa gizani.
Ili kukabiliana na tatizo hilo ushauri ulitolewa na TANESCO nasi tukaukubali kuwa wakodishe mitambo ya kuzalisha umeme kutoka nje. Serikali tukaombwa kugharamia ukodishaji huo. Taratibu za kisheria zikafanywa, tenda zikatangazwa na washindi wakapatikana Aggreco, Richmond na Alstom. Kampuni za Aggreco na Alstom zilileta mitambo yao kwa wakati lakini kampuni ya Richmond ikawa inasuasua. Wakati huo huo maneno mengi yakawa yanazagaa kuhusu Richmond kutostahili kupewa tenda kwa sababu ya kutokuwa na uwezo kwa kampuni hiyo na kampuni hiyo kutokuwa hai. Ikadaiwa kuwa wamepewa tenda kwa sababu ya kubebwa na baadhi ya viongozi Serikalini. Maneno hayo yalifanya Wizara ya Fedha wasite kutoa fedha za kuanzia kwa kampuni hiyo. Aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini wakati ule alipokuja kuniomba niingilie kati ili kampuni hiyo ilipwe malipo ya awali (down payment) nikataa na kumwambia Waziri aachane nao kwani kampuni hiyo ni ya mashaka. Hivyo kampuni ya Richmond haikulipwa down payment, wakashindwa kutimiza mkataba. Maneno yakazidi kadri makali ya kukosa umeme yalivyoendelea kuuma.
Baada ya hapo kampuni ya Richmond ikauza mkataba wake kwa kampuni ya Dowans ambayo ilileta mitambo na uzalishaji wa umeme ukafanyika na kupunguza kabisa makali ya mgao. Tuhuma kuhusu Richmond ziliendelea kulindima mpaka hatimaye Tume ya Bunge ikaundwa na kugundua kuwa Kampuni iliyouziwa haikuwa hai na ni ya mfukoni. Hatima ya Tume hiyo tunaijua sote. Aliyekuwa Waziri Mkuu na Mwawaziri wawili waliwajibika. Zile tuhuma za yeye kuwa ndiye mwenye kampuni hazikuthibitika lakini aliwajibika kwa sababu yeye ndiye aliyetoa kauli ya kukubali ipewe tenda ili kuepusha nchi isiwe gizani.
Miezi kadhaa baadaye, likazuka sakata la Dowans ifutiwe mkataba kwa hoja kuwa wamerithi mkataba na kampuni ambayo haikupata kihalali mkataba wake. Kamati ya Bunge ilisema hivyo na wanasheria wa TANESCO pia walishauri hivyo. TANESCO ikavunja mkataba. Dowans hawakuridhika, wakashitaki kwenye Baraza la Usuluhishi kama yalivyo masharti ya mkataba waliotiliana sahihi. Madai yamesikilizwa na TANESCO imeonekana ni mkosaji hivyo wakatozwa fidia ya Dola za Marekani 64 milioni.
Taarifa hiyo imetushtua wengi. Niliuliza na kupewa ushauri mbali mbali. Wapo
waliosema lazima tulipe, wapo waliosema tusilipe, wapo waliosema tusiharakishe kulipa kwani kuna uwezekano wa kutokulipa kwa kutumia sheria. Uamuzi wangu ukawa tusiharakishe kulipa, tutafute njia za kuepuka katika kulipa. Ndiyo maana ya taarifa ya Mheshimiwa Chiligati na ile ya Waziri Mkuu.
Ni mzigo mkubwa mno kwa TANESCO kubeba, hivyo tufanye kila tuwezalo tuepuke kulipa. Tumewataka wanasheria wetu wasaidiane na wale wa TANESCO kuhakikisha hilo halitokei. Nataka kuwahakikishia kuwa na mie ni miongoni mwa wale wasiotaka TANESCO ilipe, hivyo kauli za kuhusika na Dowans inanishangaza maana nisingeamua hivyo katika Kamati Kuu na Kamati ya Wabunge wa CCM. Ama kweli akutukanae hakuchagulii tusi.
"