Adverts

Feb 4, 2011

TANZANIA YAFANYA VEMA .......

TANZANIA YAFANYA VEMA .......: " Ikulu
NA MWANDISHI MAALUM Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka historia ya kuwa nchi ya kwanza duniani kuandaa Mpango wa Pamoja wa Maendeleo kwa kushirikiana na Mashirika Manne yaliyo chini ya Umoja wa Mataifa (UM).
Mashirika hayo ni Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP), Shirika la kuhudumia watoto (UNICEF), Mpango wa Chakula Duniani(WFP) na Shirika linalohusika na Idadi ya watu (UNFPA).
Kufuatia kukamilishwa kwa mchakato huo wa aina yake, Jumuia ya Kimataifa imeipongeza na kuisifu Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuonyesha njia na kuwa mfano wa kuigwa na mataifa mengine.
Mpango huo ambao unajulikana kama Common Country Programme Document (CCPD), Umewasilishwa mbele ya Bodi tendaji za UNDP na UNFPA na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Uchumi, Dkt. Servacius Likwelile. Ukiwa ni sehemu ya Mpango Mkubwa wa Umoja wa Mataifa ( UNDAP).
Bodi Tendaji za Mashirika hayo manne zinafanya mikutano yao ya kikazi katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York.Ambapo Tanzania ilipatiwa fursa ya kuwasilisha Mpango huo.
Utekelezaji wa CCPD utafanyika kwa miaka minne kuanzia Julai 2011 hadi June 2015. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia mpango huo itapata Dola za Kimarekani 773 milioni zitakazotolewa na Umoja wa Mataifa.
Akiuwasilisha CCPD Naibu Katibu Mkuu anasema, maandalizi na utekelezaji wake umezingatia vipaumbele na mipango ya maendeleo ambayo Serikali zimeainisha kupitia MKUKUTA kwa Tanzania Bara na MKUZA kwa Tanzania Visiwani.
“ Ingawa tumeshirikiana na mashirika hayo tangu hatua zote za maandalizi hadi utekelezaji wake, huu ni mpango wetu, tunaumiliki wenyewe na tumehakikisha unakidhi vipaumbele ambavyo Serikali zimejiwekea katika kuharakisha maendeleo ya wananchi wake” anasema Dkt. Likwelile.
Anaongeza kuwa maandalizi hayo pia yamewashirikisha wadau wengine zikiwamo asasi zisizo za kiserikali.
Dkt. Likwelile anasema kwa Tanzania kuwasilisha mpango huo katika Bodi tendaji za Mashirika hayo, kumeipa fursa nchi ya kutoa uzoefu wake kwa nchi nyingine wa namna ya mchakato mzima ulivyofanyika.
“ Lakini hii pia ni changamoto kwa UM, kwa sababu kwanza, hawakutegemea kwamba tungefikia hatua hii, tumewaonyesha njia, na tunawapa changamoto ya kuwa sasa wana mahali pa kuanzia katika kuboresha mfumo wa utendaji katika ngazi ya nchi”, anasisitiza Naibu Katibu Mkuu.
Akasema kuwa Mpango unaweza kutumika kama mwongozo kwa UM kama ulivyo au kwa kuuboresha kwa kuzingatia mahitaji na malengo ya nchi husika.
Akielezea manufaa ya kuwa na CCPD,Dkt Likwelike anayataja manufaa yake kuwa ni pamoja na kuboresha utendaji kazi, utekelezaji, ufuatiliaji, ufanisi katika matumizi ya raslimali fedha.
Manufaa mengine ni kujenga uwezo wa raslimali watu ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa ili kwa pamoja waweze kukabiliana na changamoto za kuleta maendeleo.
Kupitia CCPD, sasa inakuwa rahisi kujua nani anafanya nini na katika eneo gani, na itasaidia kupunguza muingiliano wa shughuli kati ya Shirika moja na jingine na kwa upande mwingine Serikali itaondokana na urasimu na ukiritimba wa kufanya kazi na shirika moja moja.
Maeneo yatakayonufaika na mpango huo ni Mazingira, HIV/AIDS,Elimu, Afya, Ukuaji wa Uchumi, Utawala Bora na Masuala ya Wakimbizi.
Bi Anne Webster kutoka Ubalozi wa Ireland, akizungumza kwa niaba ya mataifa 17 anasema.
“ Kama marafiki wa maboresho ya mfumo wa UM, na baada ya kufuatilia kwa makini mchakato wote huu. Tumeridhishwa sana na kazi iliyofanywa.Tunapenda kutambua na kuipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hatua hii ya kihistoria”
Nchi hizo ni Japan, Sweden, Uingereza, Ujerumani, Jumuia ya Ulaya, India, Canada, Finland, Belgium, Denmark,Netherelands, Norway, Ireland, Ufaransa, Spain, Switzerland na Marekani.
Akasema nchi hizo zinaunga mkono kwa dhati Mpango huo kwa sababu unaifanya Tanzania kuwa mshirika mkubwa wa UM katika maeneo muhimu ya Maendeleo.
Watendaji Wakuu wa Mashirika ya UNDP Bi Helen Clark na UNFPA Dkt. Babatunde Osotimehin, nao kwa nafasi zao walitumia fursa hiyo kuutambua, kuupokea na kuipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuukamilisha, lakini pia kwa hatua mbalimbali za maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa.
"