Makamu wa raisi wa TBF Phares Magesa akisini mkataba wa udhamini wa TBF Taifa Cup na Meneja wa bia ya Castle Lite Pamela Kikuli katika ofisi za TBL.
Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia Bia yake ya Castle Lite, leo imetangaza udhamini wa mashindano ya mpira wa kikapu yatakayofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 11/12/2011 hadi tarehe 17/12/2011.
Akizungumzia udhamini huo Meneja wa Bia ya Castle Lite Bi. Pamela Kikuli alisema; “Tunafurahi sana kupata nafasi hii ya kudhamini mashindano haya muhimu, tumeamua kushirikiana na Shirikisho la mpira wa Kikapu Tanzania (TBF) kuhakikisha mashindano haya yanafanyika katika hali ya ufanisi mkubwa. Mchezo wa mpira wa kikapu umekuwa na mvuto mkubwa na kuendelea kujizolea mashabiki wengi hapa nchini na Ulimwenguni kwa ujumla. Zaidi ya kuwa chanzo kizuri cha ajira kwa vijana, mchezo huu pia unatoa fursa kwa washiriki kufanya mazoezi ya kutosha na hivyo kuwa na afya bora wakati wote”.
Bia ya Castle lite ambayo inawalenga na kuhamasisha zaidi watu wanaojali afya zao, imeamua kuonesha hayo kwa vitendo kwa kudhamini mashindano haya na kuhakikisha inashirikiana na vyombo husika kuhakikisha kuwa mchezo wa mpira wa kikapu unakuwa hapa nchini. Aliongeza Bi. Pamela.
Akizungumzia thamani ya udhamini, Bi Pamela alisema; Castle Lite imetoa jumla ya shilingi Milioni Ishirini na Nane (28,000,000/-) ili kufanikisha mashindano haya. Tuna imani kuwa fedha hizi zitatumika vema katika maeneo yaliyokusudiwa ili kuleta tija katika mchezo huu wa mpira wa kikapu na tutaendelea kuwa mstari wa mbele kuendeleza mchezo wa kikapu hapa nchini.
Nae meneja mahusiano na habari wa TBL Bi. Edith Mushi akitaja mikoa itakayoshiriki alisema mashindano hayo kwa mwaka huu yatashirikisha mikoa 19 ya Tanzania Bara na Visiwani, ambayo ni ILALA, KINONDONI, TEMEKE (IKIWA NI MIKOA MIPYA YA KIMICHEZO YA DAR-ES-SALAAM), ARUSHA, KILIMANJARO, TANGA, ZANZIBAR, PEMBA, LINDI, MTWARA, MBEYA, IRINGA, MOROGORO, MANYARA, MARA. MWANZA, SHINYANGA, TABORA NA RUKWA.
Alisema mashindano hayo yatashirikisha timu za wanaume na wanawake na yanatarajiwa kuwa na msisimko mkubwa miongoni mwa jamii ya wanamichezo kote nchini. Mashindano haya pia yatakuwa ni sehemu ya kusherehekea miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika kwa upande wa mpira wa kikapu.
Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania Bw. Phares Magesa, alitoa shukurani na pongezi nyingi kwa Bia ya Castle Lite kwa ushirikiano mkubwa waliotoa kwa kudhamini mashindano haya ya mwaka 2011 yatakayoshirikisha timu 24 kutoka mikoa 19 ya Tanzania. “Castle Lite imeonesha moyo wa Uzalendo kwa kuwa mstari wa mbele kudhamini mashindano haya, kwa kushirikiana na mdhamini huyu tuna imani kubwa kuwa mchezo wa mpira wa kikapu utapata msukumo mkubwa utakaoleta maendeleo ya kweli katika mchezo huu hapa nchini; Alisema Magesa.
Sisi viongozi wa shirikisho na wapenzi wa mpira wa kikapu hapa nchini, Tuna imani kubwa kuwa udhamini huu utaongeza chachu ya ushindani kwa timu zitakazoshiriki na hivyo kuongeza tija katika mchezo huu hapa nchini. Tunawaomba wapenzi na mashabiki wa mpira wa kikapu kujitokeza kwa wingi katika viwanja viliyvotajwa ili kuja kushuhudia na kushangilia timu zao wakati wote wa mashindano.
Amesema udhamini wa Castle Lite utalenga maeneo yafutayo - kwanza tumezipa kipaumbele sana timu zinazotoka nje ya Dar es salaam kwa kuzisaidia fedha kiasi za kujikimu ambapo bajeti itagharimu kiasi cha Tzs milioni 22,400,000/ ikiwa ni kiasi cha TShs. 900,000.00 kwa kila timu itakayoshiriki kutoka nje ya Dar-es-Salaam. Zawadi ikiwa ni pamoja na fedha taslimu – TSh. 2,000,000.00; Vikombe kwa washindi wa kwanza na wa pili pamoja na mchezaji bora na medali kwa mshindi wa kwanza, vitagharimu Tzs Milioni 1,200,000/. Gharama za kulipia viwanja zitakuwa ni Tzs 3,000,000/; Malipo ya waamuzi ambayo imetengwa Tzs Milioni 2,100,000/; T-Shirts kwa washiriki wote TSh. 3,000,000.00. Jumla ya mchanganuo huu ni TShs. 33,700,000.00. Alisema TBF itachangia kiasi cha Shs. 5,700,000.00 za ziada toka katika vyanzo vingine.
Tunaomba ieleweke kuwa gharama hizi hazitoshi kukidhi mahitaji yote ya kuendesha mashindano la Taifa Cup lakini tunaishukuru TBL kupitia Bia ya Castle Lite kwa udhamini huu ambao umeonesha njia, na tunawashukuru mikoa yote iliyokubali kushiriki katika mashindano haya kwa kujitolea kwao kutafuta vyanzo vingine vya pesa kukidhi mahitaji ya ushiriki.